Thursday, August 20, 2015

TFF lawamani kuigwaya Yanga

SEIFEDDIN Jamal

MWANACHAMA wa  klabu ya  soka ya  Simba, Seifeddin Jamali marufu kama 'Sefu Simba' amelitupia lawama Shirikisho la Soka nchini Tanzania (TFF) kwa kulifumbia macho  suala la uchaguzi wa klabu ya  soka ya Yanga ambayo mpaka  sasa haijafanya uchaguzi kwa mujibu wa  katiba ya shirikisho  hilo.
 

Awali,  klabu  ya soka ya  Yanga ilitakiwa kufanya  uchaguzi mkuu mapema jana, lakini wakasikika kusogeza  mbele  hadi mwaka  huu, lakini  hata  hivyo hajafanya hadi sasa.
Akizungumza na mwandishi wa  habari  hizi, Jamali alisema, kitendo cha Yanga  kutofanya uchaguzi ili hali TFF ikibaki kimya haileti usawa  wa kikatiba na kanuni ya  shirikisho  hilo.
Alisema,  inashangaza kuona TFF imekuwa wakali kwa kuzitaka  baadhi ya klabu kufanya   uchaguzi, lakini imeshindwa kuonesha ukali huo kwa  Yanga na kuiacha ijiamulie muda wa kufanya  uchaguzi huku shirikisho likiwa kimya.
 

Jamali ambaye amewahi kuwa Mtunza Hazina wa klabu ya  soka ya  Simba katika miaka ya Themanini anakumbuka namna TFF ilipoishupalia Simba kufanya  uchaguzi ili hali haioneshi nguvu  hizo kwa klabu ya  soka ya  Yanga.
 

"TFF walionesha  nguvu nyingi katika kuitaka klabu ya  soka ya  Simba kufanya  uchaguzi, lakini inashangaza kuona  ipo kimya katika suala la kuitaka Yanga kufanya   uchaguzi, hii naona   haijakaa sawa hata kidogo".
 

"Hata  ukiangalia hivi sasa, takriban klabu  na  timu  zote za Ligi Kuu tayari  zimefanya uchaguzi kwa mujibu wa katiba  ya TFF, lakini  kwa upande wa  Yanga bado hawajafanya na shirikisho  linaonekana kukaa kimya, hii maana yake nini?" alihoji Jamali na kuongeza.
 

"Lazima shirikisho lioneshe usawa katika kila  hatua ya kusimamia kanuni zake kama msimamizi wa  soka la Tanzania, lakini kinachooneka hivi sasa ni kama wanaigwaya Yanga".
 

Kauli ya  Jamali inakuja siku  chache ambapo  timu mbalimbali  za Ligi Kuu tayari zimekamilisha zoezi la uchaguzi, zikiwemo  Coastal Union na African Sports ambazo zimeshachagua  viongozi wao kwa mujibu wa katiba zao na ile ya TFF.
 

Katika hatua  nyingine Jamali ameupongeza  uongozi wa  Simba kwa kuendesha vyema wiki ya  Simba ambayo hitimisho lake  ndiyo inayoitwa 'Simba Day' na kusema hatua  hiyo inaendeleza umoja ndani ya klabu.
 

Alisema, Simba Day ya mwaka  huu ilifana sana na kuwafanya wanachama na washabiki wa klabu hiyo kuwa kitu kimoja, hatua ambayo imeongeza mshikamano kwa wanasimba popote walipo.
 

" Simba Day  ni siku muhimu kwa wanasimba kuongeza  mshikamano wao ambao ni muhimu kwa timu kufanya  vizuri, hivyo naendelea kuwapongeza viongozi  na kuwataka kuendelea kuhimiza  umoja ndani ya klabu ambao ni nguzo muhimu  ya ushindi wa  timu" alisema Jamali.

No comments:

Post a Comment