Sunday, August 23, 2015

Kikosi cha Kwanza Msimbazi hiki hapa



WALA  huitaji kupiga  ramli kutambua Simba inawaanzisha nani na nani katika mechi ipi. Hii ni kwa mujibu wa mechi ambazo   Wekundu hao wameshacheza  hadi leo hii.

Hata kama   kocha Dylan Kerr hajaweka  hadharani kikosi chote cha msimu  huu, lakini  kikosi ambacho mzungu  huyo  amekuwa akikipanga kwa ajili ya kutafuta  ushindi kimeshaanza kuonekana.

Katika  mechi zote za kirafiki  ambazo Simba ilikuwa  inacheza ikiwa katika kambi ya mazoezi ya kisiwani Unguja, kocha Kerr alikuwa akianza kwa kuwapanga wachezaji  kadri alipoona ugumu na umuhimu wa mechi, lakini katika michezo tafu amekuwa akipanga  wachezaji wa kuamua matokeo ya mechi.

Kerr ambaye  msimamo wake ni kuona kila namba inakuwa na upinzani, alianza kusuka kikosi cha ushindi katika mechi tafu za kirafiki za kimataifa dhidi ya SC Villa na URA  zote za   kutoka nchini Uganda.

Katika mchezo ule wa kirafiki wa kimataifa, Kerr aliwachezesha wachezaji  wake  wote aliokuwa nao katika kambi za Lushoto  na kisha Unguja, ambapo katika kila namba kulikuwa na wanandinga wawili waliocheza katika kiwango  sawa na kuwafurahisha wanazi wa klabu hiyo waliofurika kisawasawa.

Ukiondoa mlinda mlango Vincent Angbang aliyedaka  vyema na kuwa tegemeo,  kocha Kerr aliwabadilisha namba wachezaji wengi na kuthibitisha kinachoitwa kuwa na  vikosi viwili katika kikosi  cha msimu  huu.

Kikosi cha kwanza kinachoweza kucheza katika ligi ijayo kinaweza kupangwa kwa  langoni kulindwa na  Vincent Angban, Hassan Kessy, Mohamed Hussein 'Tshabalala', Hassan Isihaka, Juuko Murshud, Justice Majabvi,Mwinyi Kazimoto, Said Ndemla, Hamis Kiiza 'Diego', Mussa Hassan Mgosi, Peter Mwalyanzi.

Katika hiki, Kocha Kerr aliwaanzisha takriban wachezaji wote hao, isipokuwa  Mwinyi Kazimoto aliyeingia baadae na kisha Mwalyanzi (Peter) alitolewa katika kipindi  cha pili.

Kwa upande wa  kikosi cha  pili, ni dhahiri langoni atasimama, Manyika Peter 'Junior' Emery Munibona, Samir Haji Nuhu, Mohamed Faki, Abdi Banda, Jonas Mkude, Issa Ngao, Awadh Juma, Danny Lyanga,  Boniface Maganga na Ibrahim Ajib.

Waliohudhuria mechi ya  'Simba  Day dhidi ya SC Villa watakuwa mashuhuda  kuwa, kocha Kerr aliwabadilisha wachezaji wake kwa mfumo wa kucheza mpira wa kasi na kila mchezaji alipewa  jukumu lililofanya wachezaji wa kikosi  kilichopangwa awali na kilichomaliza kuonekana wakiwa katika viwango  sawa kwa spidi ya mchezo, kumiliki mipira na  kuwa na safu ya ulinzi imara.

Akizungumza  na mwandishi, Kerr alisema, kwa kiasi fulani amekamilisha hatua ya kwanza ya kuangalia uwezo wa kila mchezaji  pamoja na mfumo wa kucheza  uwanjani.

Alisema, katika  hilo, amefanikiwa kuwa na  wachezaji wawili wawili katika kila idara na ndiyo maana kila aliyeingia kushika nafasi alionekana kumudu  vyema majukumu aliyopewa.

"Nilikuwa ninamwangalia kila mchezaji na sasa nimejiridhisha katika suala la kila namba kuwa na wachezaji wawili wawili. Nimeridhika na kila mchezaji na kazi iliyopo sasa ni kuendelea kuangalia  suala la nani acheze na nani" alisisitiza Kerr.

No comments:

Post a Comment