Thursday, August 20, 2015

Mrithi wa Mavugo apeta Msimbazi


KOCHA  wa  timu ya soka ya  Simba, Dylan Kerr wala  hataki kumung'unya maneno kwa  Kelvin Ndayisenga kwa kukiri kuwa straika  huyo ana mambo mengi  yanayompa nafasi ya kufuzu majaribio yatakayomfanya awe miongoni mwa wachezaji watakaosajiliwa  msimu huu.
 

Ndayisenga ambaye ni kama mrithi wa nafasi ya mrundi mwenzie, Laudit Mavugo, alikuwamo katika kikosi cha Simba kilichotoka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya URA ya  Uganda,  katika mechi iliyochezwa  Jumamosi iliyopita katika dimba kuu la Taifa, jijini Dar es Salaam.
 

Straika huyo mwenye  umbo  la wastani alionesha kiwango cha kuanza kumshawishi kocha Kerr hasa baada ya kuanza kufungua akaunti yake ya mabao akiwa na kikosi cha Wekundu wa Msimbazi kwa kufunga bao la kuongoza la kipindi cha kwanza.
 

Akizungumza na mwandishi wa  habari hizi, kocha   wa wekundu hao alisema,  straika huyo ana sifa  za kuitwa mshambuliaji  kwani anatumia  vyema mwili na akili zake awapo katika  eneo la kufunga, hivyo ameanza  vyema majaribio.
 

Alisema, goli alilofunga  dhidi ya  URA lilikuwa ni la kutumia akili zaidi kwasababu alikuwa  mbele ya mabeki wawili na mlinda mlango na alichokifanya ni ziada ya kutumia  vyema utulivu na kuangalia umbali  uliopo baina ya mlinda mlango na walinzi wake, ndipo alipofunga bao zuri.
 

Aliongeza kuwa, kutokana na hali hiyo, ana asilimia  kubwa ya kupewa  nafasi ya kuitumikia  Simba, ingawa  bado benchi ufundi linaendelea kumfanyia tathimini kabla ya kujiridhisha zaidi katika mazoezi ya kila siku kabla ya kuanza kwa ligi.
 

"Bado tunaendelea kumwangalia katika mazoezi ya kila siku, lakini katika mchezo wake wa kwanza  wa kimataifa dhidi ya  URA alicheza katika kiwango cha kuvutia"
 

"Ameanza  vizuri, ni mchezaji anayejiamini kucheza katika  nafasi ya  ushambuliaji na ameonesha  kutambua majukumu yake katika  timu kama Simba".
 

"Ingawa ni mapema kusema lolote  juu yake, ninachoweza kusema kwa  sasa ni kwamba kama atacheza  kwa  stahili ya kujituma na kutumia kila nafasi anazopata  kwa kufunga ni sawa na kusema  kuwa anasimilia kubwa ya kufuzu majaribio". alisema Kerr na kuongeza.
 

" Nimekuwa  nikisisitiza  kila  siku juu ya utaratibu wangu wa kuanza kumwangalia mchezaji kabla ya kujiaminisha juu ya  uwezo na kiwango chake cha uwanjani, hivyo  tutaendelea  kujiridhisha kwa straika  huyo na tutakuwa na majibu katika siku  chache  zijazo".
 

Awali, kocha  huyo  raia wa  Uingereza aliuagiza  uongozi kuendelea  kutupa ndoano za usajili kwa kuzingatia zaidi nafasi ya kupata straika wa kiwango  cha juu kwa ajili ya kuongoza  safu ya ushambuliaji baada ya kukwama kwa  mpango wa  Wekundu hao wa kumleta nchini mfumania nyavu Laudit Mavugo.
 

Iwapo Kelvin Ndeyisenga  atasajiliwa, atakuwa ndiye mrithi wa nafasi ya Mavugo ambaye  mpango wa kutua katika kikosi cha Wekundu wa Msimbazi ulikwamishwa na klabu yake  ya sasa ya Vital'O' kuitaji dau la dola 110,000  ambalo ni sawa na takriban shilingi 220 milioni. 

No comments:

Post a Comment