Sunday, August 23, 2015

Kerr amkubali Msenegal, awakabidhi Mwadui


HUU utakuwa mwisho wa  ubishi kama anafaa kusajiliwa au la! Kocha Mkuu wa timu ya  soka ya Simba tayari ameshuhudia kiwango cha awali  cha straika raia wa Senegal, Papa  Niang aliyetua jijini Ijumaa  kwa ajili ya majaribio. Lakini amesema kipimo zaidi itakuwa katika mechi ya dhidi ya timu ya Mwadui.

Timu ya  Simba inatarajia kushuka   katika  dimba kuu la Taifa, jijini  Dar es Salaam, Jumatatu (kesho) kujipima na timu  ya Mwadu inayonolewa na kocha  asiyeishiwa maneno, Jamhuri  Khwelo ‘Julio’, hivyo mchezo huo umepangwa kuwa kati ya mtihani wa majaribio kwa msenegal huyo.

Katika mazoezi ya Jumamosi asubuhi yaliyofanyika katika uwanja wa Maveterani wa Boko, Kerr alimwangalia Niang katika kila  hatua, kisha akawa anaandika kila jambo katika kitabu  chake  cha kumbukumbu, kisha mara kadhaa akiwa anamnong’oneza jambo msaidizi wake Seleman Matola.

Kerr alisema, atautumia mchezo huo kama kipimo cha awali cha kuendelea kujiridhisha na kiwango alichonacho msenegal  huyo ambaye  ana udugu wa kinasaba na mfumania nyavu tegemeo nchini Senegal, Mamadou Niang  aliyekuja nchini Tanzania kucheza na Taifa Stars na kuisumbua vyema ngome ya ulinzi.

“Ni mchezaji  mwenye jina na hata kiwango alichokionesha katika mazoezi ya  leo asubuhi (jana) ni kikubwa, lakini  bado tunahitaji kuendelea  kuona  zaidi  kazi yake  katika mazoezi yetu yajayo tukiwa  kisiwani Zanzibar”.

“Lakini pia tutampa nafasi  ya kuonesha kiwango chake katika mechi ya kirafiki tutatakayocheza Jumatatu (kesho) na  timu ya Mwadui. Huu utakuwa muda mwingine sahihi wa kumwangalia kwasababu tunacheza na timu ambayo bado siijui ila nasikia wana wachezaji wengi wazoefu wa ligi ya Tanzania”.

“Wate  tutakuwa uwanjani na kila jicho litashuhudia kiwango cha Niang na baadae tutakuwa naye katika  kambi  tutakayokwenda kuiweka kisiwani  Unguja,  kule  tutakuwa naye kwa  siku  tano hivi kabla  sijatoa jibu la ama asajiliwe au la!” alisema Kerr na kuongeza.

“Lengo langu ni kupata mchezaji wa nafasi ya ufungaji atakyeitendea haki  idara  hiyo, siyo kwa kubahatisha, bali kwa kazi atakayoionesha uwanjani. Sitaki kufanya  usajili  wa  kubahatisha, kwani  unaweza kuigharimu timu. Ndiyo maana nimetaka kumuona kila mchezaji kabla  ya kupeleka  jibu kwa  uongozi kama anastahili kusajiliwa au kuachana naye”

Mshambuliaji Papa Niang, raia wa Senegal aliyezaliwa Desemba 5, 1988, sasa ana miaka 26  ametua jijini Dar es Salaam akiwa ni mchezaji  huru baada ya kumaliza mkataba wake wa kuitumikia timu ya CF Mounana ya  nchini Gabon ya Magharibi mwa  bara la Afrika.

No comments:

Post a Comment