Thursday, August 6, 2015

MCHEZAJI WA YANGA ATUA KUKIPIGA DARAJA LA KWANZA

Hassan Dilunga 1
Klabu ya Ruvu Shooting leo imefanikiwa kumsajili aliyekuwa kiungo wa Yanga Hassan Dilunga mara baada ya mchezaji huyo kuvunja mkataba na wanajangwani kufuatia kushindwa kuelewana kati ya pande hizo mbili hatimaye mchezaji huyo kuwa huru.
Afisa habari wa Ruvu Shooting Masau Bwire amethibitisha Dilunga kusajiliwa na Ruvu Shooting ambayo msimu ujao itashiriki ligi daraja la kwanza baada ya kushuka daraja kwenye mechi yake ya mwisho ya ligi kuu msimu uliopita (2014-2015) ilipocheza dhidi ya Stand United na kupoteza mchezo ambapo moja kwa moja ikashuka daraja.
Awali klabu ya Yanga ilitoa taarifa ya kumpeleka Dilunga kwa mkopo kwenye klabu ya Stand United lakini inasemekana mpango huo ulishindikana kutokana na mchezaji huyo kutofikia makubaliano na klabu ya Stand United, hatimaye kujiunga na maafande hao wa JKT kutoka mkoani Pwani.
Lakini mpaka sasa bado haijafahamika kuwa Dilunga amejiunga na klabu hiyo kwa mkataba wa muda gani. Pindi taarifa hiyo itakapokuwa tayari, mtandao huu utakujuza.

No comments:

Post a Comment