Sunday, August 30, 2015

'Simba ni ya mvua na jua'


KOCHA Dylan Kerr amewaambia wachezaji wake jambo moja kubwa, ambalo ni hili:" Timu hii ni ya mvua na jua.Anayezembea mazoezi kwasasa imekula kwake na hana haja ya kubakia na wachezaji wavivu".

Lakini, kama vile haikutosha, Kerr alionesha kutotaka mzaha katika kusimamia mazoezi hayo kwa vitendo huku mwenyewe akiwa mfano wa kila hatua ya kujifua kwao.

Katika hali ya kutaka kukiweka sawa kikosi chake kabla ya kuanza kwa ligi ya msimu unaotarajia kuanza Septemba 12, Kerr alikiongoza kikosi chake bila kujali hali ya hewa iliyokuwapo kisiwani hapa juzi Ijumaa.

Mazoezi ya juzi Ijumaa yaliyofanyika katika uwanja wa Amaan, kocha Kerr aliwaongoza wachezaji wake kwa kuendelea kujifua huku kukiwa na hali ya hewa tete ya mvua kubwa iliyonyesha kuanzia asubuhi.

Wakati ambapo baadhi ya waliohuhudhuria mazoezi hayo wakidhani 'mziki' wa mazoezi utasimama kutokana na mvua hiyo,Kocha Dylan Kerr aliwaambia wachezaji wake 'Zege halitolala'.

Lakini, katika mazingira ya ajabu, wachezaji nao wakaonesha kuwa 'ngangari', wakafurahia hali hiyo na kuendelea na tizi la nguvu hali ambayo iliwapa raha makocha wote watatu.

Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa mazoezi hayo,Kerr alisema, amefurahia hali ya hewa iliyopo Zanzibar kwasasa, kwani inawapa changamoto wachezaji ya kujifua katika mazingira ya aina mbalimbali.

Alisema, wachezaji ni sawa na maaskari wa jeshi la ukombozi wanaopaswa kuwa tayari kufanya kazi katika mazingira yoyote kwa ajili ya kulinda heshima na ushindi wa nchi yao.

Aliongeza kuwa, amelazimika kuendelea na mazoezi katika mazingira ya mvua kwasababu timu lazima ijiandae kwa mazingira yoyote magumu na rahisi, kinachotakiwa ni kuwajengea utayari na stamina.

"Timu ni kama kikosi cha askari. Lazima wawe tayari kwa mazingira yoyote kwa ajili ya kupigania hadhi, heshima na ushndi kwa ajili ya wenzao ambao ni wanachama na washabiki wa klabu ya Simba" alisisitiza Kerr.

Kikosi hicho Dylan Kerr kipo kisiwani Ungujakujiandaa na Ligi Kuu ya msimu huu inayotarajia kuanza kutimua vumbi Septemba 12 mwaka huu ambapo itafungua pazia dhidi ya African Sports ya Tanga kwenye Uwanja wa Mkwakwani.

No comments:

Post a Comment