Thursday, August 20, 2015

Beki katiri Simba aanika siri nzito


Na Majuto Mbiligenda

BEKI  kisiki wa kikosi cha Wekundu wa Msimbazi Juuko Murshidi, maarufu kama ' Rio Ferdinand' ameweka hadharani kuwa  uimara wake unatokana na kutumia akili nyingi na nguvu kidogo katika kuwakabili washambuliaji wa  timu pinzani.
 

Kutokana na  hilo ndiyo maana baadhi  ya wachezaji wanadhani anacheza faulo, jambo ambalo  anapingana nalo  kwa kusema, hakuna beki yeyote  duniani anayesifiwa kama walivyo wachezaji wa  idara  zingine uwanjani.
 

Kauli ya Juuko  inakuja  siku  chache  baada ya kuisaidia  timu yake kushinda mechi mbili za kirafiki za kimataifa  dhidi ya  SC Villa na URA zote zinatoka nchini Uganda ambako ndiko alikozaliwa beki huyo.
 

Katika mechi zote mbili,  kikosi cha  Simba kiliibuka na ushindi huku Juuko akionesha kiwango  cha juu katika safu ya  ulinzi akishirikiana vyema na Hassan  Kessy ' Alves', Hassan Isihaka na Mohamed Hussein 'Tshabalala'.
 

Akizungumza na mwandishi wa  habari  hizi, Juuko alisema, kinachoonekana kama anacheza   kibabe ni aina ya uchezaji wake wa kucheza kwa kutumia nguvu kidogo na kwamba  hiyo ndiyo sifa ya mchezaji  yeyote anayecheza kama beki wa kati.
 

Alisema, mchezaji wa  safu ya ulinzi kamwe  hawezi kusifiwa kwa kucheza kama mshambuliaji na ndiyo maana kuna msemo  wa kwamba 'beki  hasifiwi' bali hulaumiwa  pindi anapopitwa na timu pinzani kushinda.
 

Aliongeza kuwa, aina ya  uchezaji wake unawapa hofu washambuliaji wa  timu pinzani kwasababu ya stamina aliyonayo, huku akimwaga  sifa kemkem kwa kocha wa mazoezi ya viungo, Dusan Momcilovic na kusema amemuongezea  nguvu na mbinu za kuhimili mikikimikiki ya washambuliaji wa  timu pinzani.
 

"Ukiniangalia ninavyocheza  utapata jibu kuwa huwa natumia akili nyingi na  nguvu kidogo wakati ninapomkabili  mchezaji wa timu pinzani, hapo ndipo utakaposikia ninacheza  kibabe jambo ambalo siyo kweli".
 

"Hata  hivyo  lazima  watu watambue kuwa mimi ni mchezaji wa  idara  ya ulinzi, lazima niwe na nguvu nyingi za kukabili mikikimikiki ya wachezaji wa  safu ya  ushambuliaji, nikicheza legelege sitakuwa na sifa za kuwa  beki imara katika kikosi cha  timu yangu".
 

"Lakini kubwa ambalo wengi hawajui ni kwamba mchezaji  anayecheza nafasi ya ulinzi hayumo katika orodha  ya wachezaji wanaoweza kusifiwa, kwani beki hawezi kusiwa  hata  siku moja" alisisitiza Juuko na kuongeza.
 

"Lingine ni kwamba, kocha wetu wa mazoezi,Dusan Momcilovic ametuongezea stamina  za kutosha msimu huu  ambapo  kwasasa kila mchezaji ana uwezo wa kucheza  hata  dakika 120 bila ya kuchoka, tofauti  hal ilivyokuwa msim  uliopita ambao baadhi ya wachezaji walikuwa wanaonekana wanachoka mapema kipindi cha pili".
 

Juuko ndiye aliyeifungia timu ya  Simba  bao la pili katika mchezo wa  Jumamosi iliyopita  dhidi ya timu ya  Watoza Ushuru wa Uganda, URA, ambapo Wekundu hao  walitoka na ushindi wa mabao 2-1 huku bao la kwanza likipachikwa  nyavuni na straika  mpya Kelvin Ndayisenga, raia wa  Burundi.

No comments:

Post a Comment