Wednesday, September 23, 2015

Yanga wasalimu amri, kusaini mkataba na Azam TV


HATIMAYE Mwenyekiti wa Yanga SC, Yussuf Manji amemaliza tofauti zake na kampuni ya Azam TV na kukubali klabu kusaini mikataba yote ya kampuni hiyo, mali ya Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa na familia yake.
Habari ambazo mwanasokablog.com imezipata kutoka ndani ya Yanga SC, ni kwamba klabu hiyo sasa inatarajiwa kusaini Mkataba wa haki za Televisheni wa Azam FC na pia wa kipindi cha Yanga TV, ambayo kwa pamoja itawafanya wapokee si chini ya Sh. Milioni 600 za ‘chap chap’.
Mechi za Yanga SC zimekuwa zikionyeshwa kama kawaida na Azam TV, lakini kwa miaka yote miwili klabu haijachukua mgawo wake Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Julai 29, mwaka 2013 Manji alipinga vikali TFF na Bodi ya Ligi kuamua peke yao kuingia Mkataba wa miaka mitatu Azam TV akidai haijawahi kutokea katika ligi ya mpira wa miguu ya kisasa kulazimishwa kwa Klabu inayoshindana katika ligi kuachia haki zake za urushwaji wa michezo zichukuliwe na chombo cha habari cha Klabu ya upinzani.
Lakini pamoja na madai hayo, kuna mpango hasi wa ushirikiano baina ya na Simba na Yanga kwenda kusaini Mkataba na kampuni moja ya Kenya iliyopanga kuitibulia Azam TV.
Lakini kutokana na TFF chini ya Rais Leodegar Chillah Tenga wakati huo kusimama kidete kuitetea Azam TV iliyoweka historia katika soka ya Tanzania kwa dau lake nono, mpango huo ukafa.
Simba SC walikubali yaishe na kusaini hadi Mkataba wa kipindi cha TV ambao uliwafanya wapatiwe Sh. Milioni 331 za Mkataba wa miaka mitatu.
Yanga SC itakaposaini mikataba ya Azam TV pamoja na kupewa mgawo wa matangazo ya Ligi Kuu takriban Sh. Milioni 300 za miaka miwili, watalipwa pia na fedha za Yanga TV kwa sababu hayo ni makubaliano ya kimsingi kabla ya kusainiwa Mkataba huo.

No comments:

Post a Comment