Wednesday, September 2, 2015

Simba yaanika sababu za kutomrudisha Kiongera

Paul Raphael Kiongera

Klabu ya Simba imeeleza sababu za kutomrejesha kundini mshambuliaji wake hatari Mkenya Paul Raphael Kiongera ambaye mwishoni mwa mwaka jana alifanyiwa upasuaji wa goti India. 
Jumanne Agosti 12, 2014 Kiongera (22) alisaini mkataba wa miaka miwili kuitumikia Simba kwa dau lililoelezwa kuwa Dola za Marekani 20,000 (Sh. milioni 42), lakini akaumia na kutonesha majeraha yake ya muda mrefu ya goti katika mechi yao ya kwanza ya ligi ya Bara msimu uliopita waliyotoka sare ya 2-2 dhidi ya Coastal Union kwenye Uwanja wa Taifa. 
Kaimu Katibu Mkuu wa Simba, Collins Frisch, amesema jijini hapa kuwa hawana mpango wa kumrejesha nchini mshambuliaji huyo kwa vile tayari ana mkataba wa miezi sita kuitumikia kwa mkopo klabu ya KCB ya Ligi Kuu yta Kenya (KPL). 
“Kuna mambo mengi yanazungumzwa kuhusu Simba na Kiongera, lakini hayana ukweli. Watu wanasema Kiongera ni mgonjwa akiwa Tanzania, lakini anatupia akiwa Kenya. Hatuwezi kumrudisha kwenye kikosi chetu kwa sasa kwa sababu ana mkataba wa miezi sita na KCB utakaomalizika Desemba,” amesema. 
Mjumbe huyo wa Kamati ya Utendaji ya Simba amesema Kiongera bado ni mali ya klabu hiyo ya Msimbazi kwa muda mrefu kwani mkataba wake ulirefusha zaidi baada ya kuumia mwaka jana. 
Kabla ya kuumia, Kiongera aliichezea Simba mechi tano tu na kufunga mabao mawili. Kwa sasa anashika nafasi ya tano kwenye orodha ya wafumania nyavui hatari KPL akiwa na mabao tisa, 10 nyuma ya kinara Jesse Were (Tusker FC) anayefuatwa na mkali Micheal Olunga wa Gor Mahia mwenye mabao 15, Meddie Kagere wa Gor Mahia pia (13) na John Makwata wa Ulinzi Stars (10).

No comments:

Post a Comment