Wednesday, September 2, 2015

Klabu zaweka rekodi mpya ya usajili Uingereza

Anthony Martial mchezaji mpya wa Manchester United

Klabu za nchini Uingereza, vilivunja rekodi ya kutumia pesa nyingi zaidi katika historia ya Ligi ya Premier majira ya joto huku pesa zilizotumiwa na vilabu hivyo katika mwaka mmoja zikifika £1bn kwa mara ya kwanza.
Katika kipindi cha kuhama wachezaji kilichomalizika siku ya Jumanne, vilabu vilitumia £870m, 4% juu ya rekodi iliyowekwa mwaka uliopita.
Ukiongeza £130m zilizotumiwa na vilabu hivyo dirisha fupi Januari, kiasi hicho kinafikia £1bn.
Kilabu ya Manchester City ilitumia pesa nyingi zaidi, ikinunua wachezaji wawili bei ghali zaidi, £55m kwa Kevin De Bruyne kutoka Wolfsburg na £49m kwa Raheem Sterling kutoka Liverpool.
Usajili wa Manchester United wa £36m kumchukua mchezaji wa Monaco, Anthony Martial, ulikuwa wa juu zaidi siku ya mwisho ya kuhama wachezaji.
Gharama yake inaweza kupanda hadi £58m ukiongeza vikolezo vingine.
Tangu kuanzishwa kwa mfumo wa kuwepo kwa awamu ya kuhama wachezaji 2002, jumla ya pesa zilizotumiwa imezidi £7.3bn, zaidi ya 80% ya kiasi hicho zikitumiwa majira ya joto, kwa mujibu wa wadadisi wa kifedha wa Deloitte.
Kuhamia kwa Kevin De Bruyne, Manchester City, ndiko kulikokuwa ghali zaidi sokoni.
Manchester City walivunja rekodi ya klabu hiyo mara mbili awamu iliyopita ya usajili kwa kuwanunua De Bruyne na Sterling na kuwafanya kuwa klabu iliyotumia pesa nyingi zaidi kwa awamu moja nchini Uingereza.
Jumla ya pesa walizotumia ya takriban £160m, inazidi takriban £150m walizotumia Manchester United, majira ya joto 2014, wachezaji wengine waliowanunua wakiwa Fabian Delph, Patrick Roberts na Nicolas Otamendi.
Viongozi hao wa sasa wa Ligi ya Premia walipata afueni majira ya sasa ya joto baada ya kuondolewa vikwazo vya matumizi ya pesa walipotimiza lengo walilowekewa chini ya sheria mpya ya haki na usawa.
City walikuwa wamewekewa kiwango cha juu cha matumizi cha £49 mwaka 2014 na walitozwa pia faini ya £16.3m kwa kukiuka kanuni za Uefa.
Vilabu vinne vya Ligi ya Premier, vinavyoshiriki Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya msimu huu Manchester City, Manchester United, Chelsea na Arsenal vilitumia kwa jumla takriban £340m, ikiwa ni karibu 40% ya jumla ya pesa zilizotumiwa na klabu za Ligi ya Premier, kununua wachezaji.
Kununuliwa kwa Martial mwenye umri wa miaka 19, Everton kumnunua mlinzi wa Argentina Ramiro Funes Mori, kwa £9.5m na Papy Djilobodji kununuliwa £4m na Chelsea kutoka Nantes, siku ya Jumanne kuliwezesha awamu hii ya usajili kupita £835m zilizotumiwa mwaka jana.Liverpool wametumia pesa zaidi kuwasajili wachezaji saba, Christian Benteke (£32.5m), Roberto Firmino (£29m) na Nathaniel Clyne (£12m) wakiwa ndio ghali zaidi.
Manchester United pia wamekuwa mbioni, wakitumia £139m kununua Martial, Memphis Depay, Matteo Darmian, Bastian Schweinsteiger na Morgan Schneiderlin, huku Chelsea wakisubiri hadi dakika za mwisho kununua wachezaji wa thamani, wakiwachukua Pedro, Baba Rahman na Djilobodji.
Kilabu iliyopandishwa daraja majuzi ya Watford ndiyo iliyonunua wachezaji wengi zaidi ligini, ikiwapata wachezaji 15 wapya.

No comments:

Post a Comment