Wednesday, September 16, 2015

Sserunkuma kucheza mechi ya 30 bila bao Simba

IWAPO atapangwa katika mchezo wa leo dhidi ya Mgambo JKT Uwanja wa Mkwakwani, Tanga mshambuliaji Mganda Simon Sserunkuma atakuwa amefikisha mechi 30 tangu ajiunge na Simba SC.
Lakini katika mecho zote 29 za awali hadi sasa, Sserunkuma aliyesajiliwa msimu uliopita kutoka Express ya kwao Uganda, hajaweza kufunga hata bao moja.
Pamoja na kwamba aliachwa, lakini mshambuliaji Mganda mwenzake, Dan Sserunkuma aliifungia Simba SC mabao matano, yakiwemo matatu ya Ligi Kuu msimu uliopita katika jumla ya mechi 17.


Simon anazidiwa hata na beki Mganda mwenzake, Juuko Murushid ambaye tayari ameifungia Simba SC bao moja katika mechi 30 alizocheza hadi sasa.
Hamisi Kiiza, Mganda mwingine Simba SC aliyesajiliwa mwezi uliopita tayari ameifungia timu hiyo mabao matano katika mechi 11, likiwemo moja la Ligi Kuu.
Wazi hii ni nafasi ya mwisho kwa Simon, iwapo hataanza kuonyesha umuhimu wake ndani ya timu, ifikapo Desemba atamuachia mwingine nafasi hiyo.
Na Simon aliponea chupuchupu kuachwa mwezi uliopita, baada ya uongozi wa Simba SC kuamua kumpa nafasi nyingine wakiamini bado kijana mdogo anaweza kufufua makali.
Inaaminika Simon ni mchezaji mzuri, lakini anajiamini kupita kiasi na hataki kufanya bidii ya kucheza kwa kuonyesha umuhimu wake ndani ya timu.  

No comments:

Post a Comment